Bila kuwekeza katika kilimo,Waafrika wataendelea kuwa na njaa.
Upatikanaji haba wa maji, mafuriko ya mara kwa mara na ukame ikiwa ni pamoja na kukosekana kwa dhamira za kisiasa kuwekeza katika wakulima wadogo kunasababisha njaa katika Afrika nzima, wanasema wataalam wa usalama wa chakula.
JOHANNESBURG, Okt 24 (IPS) – Wanajibu hoja za Ripoti ya Njaa ya Kimataifa 2010 (GHI), iliyochapishwa katikati mwa Oktoba, jambo ambalo litaonyesha kuwa nchi 29 duniani zina kiwango cha njaa ambacho kinaonekana kutishia maisha. Ishirini na mbili kati ya nchi hizi – zaidi ya theluthi mbili – zinapatikana katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.
GHI – ambayo inaangalia vigezo 100-ilipima njaa kwa kujikita katika idadi ya watu wanaokosa mlo, idadi ya watoto chini ya miaka mitano ambao wana uzito duni na kiwango cha vifo vya watoto wachanga nchini humo – inachapishwa kila mwaka na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Sera za Chakula (IFPRI) na shirika la misaada la Ireland la Concern Worldwide.
Afrika imepata mafanikio kidogo katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, kutoka nafasi ya 25.3 mwaka 1990 hadi 21.7 mwaka 2010, lakini kwa kiwango hiki hakuna uwezekano wa Afrika kufikia Lengo la Maendeleo ya Milenia la kupunguza nusu ya njaa ifikapo mwaka 2015.
“Kunakosekana mafanikio,” anaonya Marie Ruel, mkurugenzi wa umaskini wa IFPRI, afya na kitengo cha lishe, akibainisha kuwa ni jambo linaloleta wasiwasi kwamba baadhi ya mataifa ya Afrika, asilimia ya watu wenye njaa imeongezeka katika kipindi cha miaka iliyopita.
Bado njaa inaendelea
Kulingana na ripoti, Jamhuri ya Kidemorkasia ya Kongo ina kiwango cha juu zaidi cha watu wanaokabiliwa na njaa duniani, ikifuatiwa na Chad, Eritrea na Burundi. DRC pia ina kiwango cha juu zaidi cha watu wenye njaa – robo tatu ya wakazi wake – na moja ya nchi yenye kiwango cha juu zaidi cha vifo vya watoto duniani.
Burundi, Comoros na Eritrea hazina nafasi nzuri zaidi, huku nusu ya wakazi wake wakiwa na njaa.
Moja ya sababu kuu za njaa katika mataifa haya ni kuendelea kukosekana kwa usalama kutokana na vita, ripoti inabainisha, lakini pia kuna sababu nyingine nyingi ambazo zinachangia kukosekana kwa usalama wa chakula, kama vile upatikanaji wa maji, kukosekana kwa vitega uchumi katika kilimo na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi.
Kwa upande wa Burundi, kwa mfano, sababu kuu ya kukosekana kwa usalama wa chakula ni usimamiaji duni wa maji, ambao unadhoofisha sekta ya kilimo nchini humo, Profesa Sheryl Hendriks, mtafiti katika Idara ya Uchumi wa Kilimo, Ugani na Maendeleo ya Vijijini katika Chuo Kikuu cha Pretoria nchini Afrika Kusini ana amini hivyo.
“Kukosekana kwa usimamiaji wa maji kuna maana kuwa nchi haina maji ya kutosha, kama ilivyo kwa Burundi, hakuna uzalishaji wa kutosha wa chakula,” anasema.
Kutokana na njaa, zaidi ya nusu ya watoto wa Burundi wamedumaa, kulingana na GHI. Madagascar, Malawi, Ethiopia na Rwanda ina viwango vinavyofanana vya kudumaa kwa watoto, wakati Chad, Angola na Somalia zinakabiliwa na viwango vya juu vya vifo vya watoto wachanga vya zaidi ya asilimia 20 kutokana na njaa.
Viwango vya chini vya uzalishaji
Kama ilivyo kwa Burundi, uzalishaji duni wa kilimo ni sababu ya kuenea kwa kiasi kikubwa cha njaa nchini Eritrea, ambako ukame na mabomu ya ardhini katika maeneo yanayofaa kwa kilimo baada ya miaka miwili ya vita na Ethiopia, ambayo ilimazilika mwaka 2000, kumesababisha kukosekana kwa usalama wa chakula, kulingana na Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP).
Katika miaka yake iliyokuwa na uzalishaji mkubwa, Eritrea ilizalisha asilimia 60 tu ya mahitaji yake ya nafaka na inategemea kuagiza chakula nje, linaripoti Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO). Katika miaka ya uzalishaji mkubwa, uzalishaji wa nafaka ulishuka kwa asilimia 25 ya mahitaji.
Vile vile, nchini Chad, kilimo, ambacho tayari ni duni kutokana na hali ya hewa kame, kimedhoofishwa na vita vya mfululizo, huku asilimia 80 ya wakazi wakitegemea msaada wa chakula, kulingana na WFP.
Vita pia vimezingira mipaka ya DRC tangu mwaka 1996, na kusababisha kupanda kwa bei kwa asilimai 52 kati ya Mei 2008 na Juni 2009, kulingana na WFP, ikiwa ni zaidi ya uwezo wa Wakongo wengi. Misaada ya kibinadamu inaendelea kubakia michache katika maeneo mengi yenye vita ya nchi hiyo, hasa katika Jimbo la Kivu Kaskazini.
Ni serikali chache tu za nchi za Kiafrika zimeweza kuboresha usalama wa chakula nchini mwao, zaidi kwa kupitia uwekezaji katika kilimo. Ghana, kwa mfano, iliweza kuboresha nafasi yake katika ripoti kutoka 23.4 mwaka 1990 hadi 10 mwaka huu, kulingana na GHI.
Hendriks ana imani kuwa Ghana ni taifa la kwanza barani Afrika kuwa njiani kufikia MDG 1.
“[Ghana] inawekeza katika kilimo, mpango wa kutoa chakula mashuleni na mifumo ya habari na kujenga uwezo,” anasema, akiongeza kuwa serikali ya Ghana pia imefanikiwa kutoa ruzuku kwa wakulima wadogo.
Ethiopia, Angola na Msumbiji pia zimepata mafanikio katika kupunguza njaa, pamoja na kwamba katika mataifa yote matatu ‘usalama wa chakula unaendelea “kuwa tishio” huku yakipewa alama 29.8, 27.2 na 23.7, kulingana na ripoti.
Hakuna ufumbuzi wa haraka
Wataalam wa usalama wa chakula wanapendekeza kuwa mataifa mengine ya Afrika yafuate nyayo za Ghana katika kuwekeza kwenye kilimo, na kuonya kuwa hakuna hatua ya haraka ya kuondokana na kukosekana kwa usalama wa chakula katika bara.
Pamoja na kwamba misaada ya muda mfupi inapambana na njaa, kwa mfano msaada wa chakula, ni muhimu kuondokana na uhaba usioonekana, serikali za Afrika zinatakiwa kulenga katika mikakati ya muda mrefu ya kukuza uzalishaji wa kilimo, anasema Dk Joyce Chitja, kaimu mkurugenzi wa Kituo cha Usalama wa Chakula Afrika katika Chuo Kikuu cha KwaZulu-Natal nchini Afrika Kusini.
“Ni muhimu kuhakikisha kuwa mipango ya kuondokana na njaa na misaada ya chakula inaondolewa polepole kwa kufanya uzalishaji wa kilimo kuwa wa kawaida,” anaelezea, akibainisha kuwa serikali zinahitaji “kufufua na kuanzisha tena uzalishaji wa kilimo”.
Hendriks anakubaliana kuwa kukosekana kwa usalama wa chakula katika bara kunaweza kutatuliwa tu kama nchi za Afrika zitazalisha chakula cha kutosha kulisha wakazi wake: “Ufumbuzi wa kukosekana kwa usalama wa chakula barani Afrika utategemeana na uzalishaji wa kilimo cha mazao, mifugo na uvuvi, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa masoko na miundombinu.” (END/2010)
Chanzo; Chris Stain